Saturday, November 10, 2012

Breaking News

MASIKINI AFANDE CHACHA

AJIMALIZA KWA RISASI KISA TOFALI

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Katavi, Dhahiri A. Kidavashari
ASKARI mmoja wa jeshi la polisi mkoa wa Katavi amefariki dunia papo hapo baada ya kujipiga risasi mchana leo Novemba 10, 2012 katika eneo la Nsemulwa kwa Mkumbo mjini Mpanda.

tukio hilo limetokea katika eneo linalotumika kufyatulia tofali ya kujengea ambapo imeelezwa kuwa askari aliyejiua ametajwa kwa jina moja la Chacha wa kikosi cha kutuliza ghasia mjini Mpanda baada ya kukuta mama mmoja akisombelea tofali alizokuwa amenunua kutoka kwa muuzaji wa tofali.

Kaimu kamanda wa jeshi la polisi mkoa wa Katavi, Joseph Myovella amesema askari huyo alikuwa katika shughuli binafsi majira ya mchana alikwenda kuangalia tofali alizonunua katika mtaa wa Nsemulwa kwa Mkumbo na alipofika katika eneo alilonunulia tofali alimkuta mama mmoja akisombelea tofali hizo kwa madai kuwa ni za kwake na yeye ameuziwa tofali hizo ndipo askari huyo alirejea kituo cha polisi Mpanda mjini na kuchukua silaha aina ya SMG na kuondoka kuelekea alikokuwa amenunulia tofali.

imeelezwa kuwa alipofika eneo la tofali alimkuta mama huyo akiendelea na kazi ya kusomba tofali ndipo alimpiga risasi tatu tumboni, kifuani na ubavuni na kisha akapiga simu kituo cha polisi na kueleza kuwa ameua mtu na yeye anajiua

baada ya kupiga simu askari huyo alijipiga risasi sehemu za koromeo, kidevuni na sehemu za kifuani na kufariki papo hapo

hali ya majeruhi imeelezewa kuwa bado ni mbaya anaendelea kupata huduma katika hospitali ya wilaya ya Mpanda.

HABARI NJEMA ZA MKOA WA KATAVI HIZI HAPA

Miezi Kumi na Miwili ya kongamano La Uwekezaji Katavi

Mnamo Oktoba 17, 2011 Mji wa Mpanda  ulipokea wageni mbalimbali kutoka ndani na nje ya nchi waliofika kwa lengo la kushiriki katika Kongamano kubwa la Kimataifa la Uwekezaji ambalo mwenyekiti wake alikuwa Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. Jakaya Mrisho Kikwete.
Hali ya maboresho ya kisekta baada ya kongamano la uwekezaji lililofanyika Oktoba 17, 2011 katika Halmashauri ya Mji Mpanda katika kipindi cha mwaka mmoja hadi Novemba 2012 ni kama ifuatavyo:-.
Katika Halmashauri ya mji Mpanda uwekezaji umekuwa ukiongezeka katika kipindi cha mwaka 2011/12 kutokana na takwimu za maombi ya leseni na maeneo ya uwekezaji kuongezeka kutoka waombaji wa leseni za biashara 40 katika mwaka wa fedha 2010/11 hadi waombaji 211 wa leseni za biashara mbali mbali katika kipindi cha Oktoba 2011 hadi Julai 2012. 
 Kuanzia julai 23, 2012 kitabu cha leseni kilichokuwepo kiliisha ambapo maelekezo ya wizara yalielekeza kuwa halmashauri zisubiri utaratibu mpya wa leseni za biashara utakapotolewa. 
Leseni zilizoombwa ni kwa ajili ya duka la dawa leseni mbili, kuuza misumari leseni moja, spea za baiskeli leseni nne, kibanda cha simu leseni moja, kuuza Oil leseni moja, Nyumba ya kulala wangeni leseni nne, mgahawa leseni mbili, kuuza vocha  leseni nne, wakala wa M-pesa leseni tatu, duka la reja reja leseni 25 na vyombo vya nyumbani leseni nane

Maombi mengine yalikuwa leseni ya stationary supplies, vyuma chakavu, mitumba, nguo, viaa vya ofisini, ushuru wa mazao, kituo cha kurusha matangazo ya radio ya fm, usafirishaji, vyombo vya pikipiki, vioo na vifaa vyake, vifaa vya radio na runinga, vifaa vya ujenzi, vifaa vya magari, mashine ya kusaga, kuuza gesi na mitambo yake ya kupikia, kununua na kuuza ng’ombe na mashine ya kusaga
     
Pia ziliombwa leseni za zahanati, udalali, uwakili, bima ya mali, bucha pamoja na kuuza simu za mkononi
Aidha latila sekta ya mawasiliano kumekuwa na maboresho makubwa ya mawasiliano kwa kutumia mitandao ambapo kuna zaidi ya blogs ishirini na mbili katika mkoa wa Katavi hususani mjini Mpanda kati ya hizo tano zinamilikiwa na kuendeshwa na waandishi wa habari waliopata mafunzo ya uendeshaji wa blogs, mbili zinamilikiwa na Halmashauri na hivi sasa inatayarishwa website ya mkoa wa Katavi baada ya kukamilika kwa website ya Halmashauri ya wilaya ya Mpanda ambayo makao yake makuu yako mjini Mpanda. 

Aidha Halmashauri ya mji Mpanda wakati inajipanga kuwa Manispaa imeanza mchakato wa kuwa na website yake mara baada ya kukamilika website ya mkoa kutokana na kuwa na wataalamu wale wale wanaoanda website kwa ajili ya taasisi za serikali ambao ni watumishi wa halmashauri mbili, ya Mji na halmashauri ya wilaya ya Mpanda. 

Katika usafiri wa anga maboresho ya uwanja wa ndege yamechangia kubadili sura ya mji wa Mpanda na kuongeza uchumi kwa wakazi wa mjini Mpanda pamoja na kuwa na uhakika wa safari za ndege baada ya kuanza kwa usafiri wa anga ambapo kampuni ya ndege ya Uric Air kuanza safari za Mpanda, Tabora, Mwanza na Mbeya, Sumbawanga, Mpanda, Iringa na Dar Es Salaam.  

Ifuatayo ni baadhi ya miradi iliyoibuliwa na wananchi, wawekezaji na wadau wa maendeleo ya mkoa wa Katavi baada ya kongamano la uwekezaji katika kipindi cha miezi kumi na mbili iliyopita katika eneo la Halmashauri ya Mji Mpanda. 

Miradi hiyo imegawanyika kisekta ambapo taarifa hii imechukua miradi wakilishi ya mingine kwani sekta moja imekuwa na miradi zaidi ya mmoja iliyoibuliwa na hivyo kuonesha sura ya mafanikio ya kongamano la uwekezaji ambalo lilifanyika kwa mara ya kwanza mjini Mpanda enzi hizo ikiwa ni mkoa wa Rukwa.
ASANTE VODACOMTZ 





DUBAI GUEST HOUSE MPANDA
 Nyumba hii ya kulala wageni ya Dubai iko katika mtaa wa Majengo kata ya Kashaulili mjini Mpanda, ilianza kujengwa  2011  ikiwa ni matunda ya msukumo wa uhitaji wa nyumba za kulala wageni zenye hadhi ya kati na ya juu katika mji wa Mpanda mara baada ya kongamano la uwekezaji. 

Mradi huu umegharimu jumla ya  Shilingi 100,000,000/= (milioni Mia moja)  zikiwa ni fedha zinazotokana na shughuli za kilimo na biashara zilizotolewa na mmiliki wa nyumba hii ni ndugu IBRAHIM MAGOHA.
 
Nyumba hii ya kulala wageni ina jumla ya vyumba 10 na inahudumia wageni wa ndani na nje ya nchi tangu ikamilike mwezi Julai 2012 

Tangu kuanza kazi nyumba hii imekuwa ikijaza wageni vyumba vyote kila siku na kuwa na uhakika wa kipato cha wastani wa shilingi 5,400,000/= kwa mwezi. 

LYAMBA LYA MFIPA VILLAGE HOTELL 

 Ni hoteli ya Kisasa iliyopo katika Mji wa Mpanda kata ya Ilembo jirani na ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Mpanda. 

Hoteli hii ilianza kujengwa mwaka 2010 na kukamilika ujenzi wa awali wa vyumba 29 vinavyojitegemea kila kimoja mnamo Aprili 2012 kutokana na msukumo wa uhitaji wa malazi kwa wageni wa kimataifa katika mji wa Mpanda Gharama za mradi huu ni zaidi ya shilingi milioni 800 ambapo ujenzi wa kumbi za mikutano na mahitaji mengine ya malazi ya wageni unaendelea Mmiliki wa hoteli hii ya kisasa ni Deusi Assenga na kampuni yake ya Assenga Association Co. Ltd ya Mpanda 

Kipato cha hoteli hii kwa wastani katika mwezi kwa vyumba vilivyokamilika kwa sasa ni shilingi 6,500,000/=(milioni sita na laki tano) 

Ujenzi wa hoteli hii ni chachu ya kuinua kipato cha Mji wa Mpanda pamoja na kuuwezesha mji wa Mpanda kupokea wageni wa aina zote bila kikwazo cha malazi ya uhakika. 


BENKI YA CRDB MPANDA 
 Kufunguliwa kwa tawi la benki ya CRDB kumetokana na hali halisi ya uhitaji wa huduma za kibenki katika mkoa wa Katavi kutokana na kukua na biashara na mzunguko wa fedha katika jamii ya wakazi wa mkoa wa Katavi. 
Tawi la CRDB Mpanda lililofunguliwa miezi miwili kabla ya kongamano la uwekezaji ni moja ya matunda ya kongamano kwani uwepo wa kongamano ni sehemu ya msukumo wa kufunguliwa mapema benki hii ili washiriki na wadau wa maendeleo waweze kupata huduma ya kibenki kutoka CRDB. 
Licha ya kuwa na uchanga katika kazi ya kibenki,  benki ya CRDB tawi la Mpanda imepeta ongezeko la wateja katika kipindi cha mwaka mmoja kutoka wateja 1,000 mwezi Septemba  2011 hadi wateja 5,700 Novemba 6,  2012 ikiwa ni ishara ya kuwepo kwa hitaji la upanuzi wa benki hii hivi karibuni kutokana na ongezeko la wateja. Changamoto inayoikabili benki ya CRDB Mpanda ni kutopatikana kwa hati za umiliki wa nyumba au ardhi kwa wateja wake ili waweze kukopesheka na kuinua kipato cha wateja wake. 


MWANANCHI DUKA LA DAWA 


 Mwananchi duka la dawa lipo katika mtaa wa kanisa la Moravian mjini Mpanda katika jengo la kitegauchumi la kanisa hilo, duka hili linatizamana na ofisi za kampuni ya mabasi ya Sumry katika soko la Buzogwe
Duka hili lilianza Juni 2012 baada ya kukamilika kwa ukarabati wa jingo ambapo mmiliki wa duka hili anaitwa Dr Lugata mkazi wa mjini Mpanda 
Maendeleo ya mauzo yamekuwa yakipanda kadiri siku zinavyosonga mbele kutokana na ugeni wa eneo husika wananchi wengi bado hawajajua kama kuna duka la dawa za binadamu changamoto ambayo mmiliki wa duka hili anasema inapungua siku hadi siku. 
Baada ya kongamano mmiliki wa duka la Mwananchi ndipo alipopata wazo la kuweka duka hilo kutokana na msongamano wa watu mjini Mpanda na kuwepo kwa mahitaji makubwa ya huduma ya dawa baridi.
 
KONGAMANO LA UWEKEZAJI LAFUFUA USAFIRI WA MABASI TABORA MPANDA 

   
Katika kile kinachoonekana kuwa ni matunda ya wazi ya kongamano la uwekezaji lililofanyika Oktoba 17, 2011 katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Mpanda bila shaka yoyote ni kuibuka kwa usafiri wa mabasi kutoka Tabora mjini hadi Mpanda mjini. 
Kwa kipindi cha miongo kadhaa kumekuwa hakuna usafiri wa bara bara kutoka mjini Tabora kuelekea mjini Mpanda kwa kutumia mabasi ya kisasa na badala yake wananchi waliokuwa wakisafiri katika ya mikoa ya Rukwa enzi hizo na Tabora walilazimika kuzunguka Mbeya au kutumia usafiri wa garimoshi. 

Mara baada ya kongamano kupita mji wa Mpanda ulianza kupokea mabasi kila siku na kuongeza idadi ya mabasi yanahudumiwa na stendi kuu ya mabasi mjini Mpanda na kuonekana kuelewa kwa stendi hiyo iliyobuniwa kwa ajili ya kuhudumia mabasi ya mikoani. 
Kila siku kuna mabasi yanayoondoka kuelekea mjini Tabora toka Mpanda na pia kunamabasi yanakuja Mpanda kutoka mjini Tabora na wakati mwingine mawili kwa siku moja na safari moja.

 WAKULIMA KAKESE WAFURAHIA GHALA JIPYA LA MAZAO YA CHAKULA


Katika kuboresha kilimo kwanza Halmashauri ya mji iliwaongoza wananchi wa Kakese kuibua Mradi wa ujenzi wa ghala ambao uliibuliwa na wananchi wa kijiji cha Mbugani Januari 2012 kupitia zoezi la fursa na vikwazo vya maendeleo (O & OD) na kuanza ujenzi mwezi Mei 2012. 
Mradi huu umegharimu jumla ya shilingi za kitanzania 62,890,000/= kwa ufadhili wa mpango wa maendeleo ya kilimo wilaya (DADPS) na baada ya kukamilika mwezi Desemba 2012 ghala hili litakuwa na uwezo wa kuhifadhi tani 250 za mpunga
Wakizungumza kijijini hapo juu ya matumaini yao katika ghala ya mazao wananchi hao walisema kuwa walikuwa wanalazimika kuuza mazao kwa ya chini kutokana na ukosefu wa ghala la kutunzia mazao pamoja na kuwa wanategemea kutumia mtindo wa kuuza mazao ya katika ghala hilo kwa kutumia utaratibu wa stakabadhi ghalani

NJIA MBILI KIVUTIO CHA MJI WA MPANDA 

Uwepo wa barabara mbili za lami kati kati ya mji ni sehemu ya kivutio cha mji wowote utofauti wa mji wa mpanda ni kuwa na mandhari nzuri ya njia mbili iliyobebwa na maua yaliyopanda kwa ustadi mkubwa  pamoja na mapambo ya matangazo ya kampuni ya simu ya Vodacom
 Vodacom Tanzania iliamua kufanya mazungumzo na Halmashauri ya mji Mpanda kuwa na maboresho ya njia mbili eneo la kati kati ya Mji maarufu kama Buzogwe ili kuwa na sura ya mji yenye mfano wa pekee baada ya kongamano la uwekezaji la oktoba 17, 2011 
Ni dhahiri kuwa bila kongamano hilo Vodacom wasingeiona barabara mbili kama inahitaji kuwekewa mabango yake na sasa imekuwa kama maua yaliyoko katika makao makuu ya mkoa wa Katavi.

BIMA YA TAIFA YA AFYA WAPATA WAKALA WAKE KATIKA MKOA MPYA WA KATAVI 
  SEMIU PHAMACY ya mjini Mpanda imeteuliwa na Bima ya Taifa ya Afya kuwa wakala wake katika mkoa wa katavi baada ya kubaini mahitaji ya mkoa huo kuwa makubwa kutokana na wingi wa mahitaji ya huduma hiyo kuwa kubwa. 
Mmiliki wa Semiu Phamacy, Adrian Siwalima alisema kuwa alianza duka la dawa oktoba 2010 lakini baada ya kupita kongamano la uwekezaji alipata wageni kutoka shirika la Bima ya afya nchi wakitaka kufanya mazungumzo naye aweze kuwa wakala wa shirika hilo katika mkoa wa Katavi.
Alisema alikubaliana nao kufanya maboresho ya jingo lake ili liweze kumudu mahitaji ya huduma husika ambapo amefanya marekebisho ya jingo na kuwa na hadhi ya Bima ya Afya kwa kufuata ramani ya shirika kwa gharama ya shilingi milioni ishirini (20,000,000
Alisema baada ya kuanza mauzo ya dawa baridi katika duka hilo la Bima mapato yamefikia shilingi milioni kumi (10,000,000) kwa mwezi kutokana na ugeni wa huduma hiyo ambapo alibainisha kuwa kwa ongezeko la watu lilivyo katikam mkoa wa katavi mauzo yatapanda mara nne au zaidi ya hapo. 



 Baada ya kongamano la uwekezaji la mwaka jana, miezi michache kumeibuka ujenzi wa mitambo ya kurushia matangazo ya radio miwili kwa masafa ya fm katika mji wa Mpanda yaliko makao makuu ya mkoa wa Katavi 
Ipo Mpanda Radio Fm inayomilikiwa na mfanyabiashara wa mjini Mpanda Aleem Kanji iliyopo katika eneo la Mpandahoteli jirani na kiwanda cha Madini cha TPM inayotarajia kuanza wakati wowote baada ya kupata kibali kutoka tume ya mawasiliano kwani ujenzi ulishakamilika bado kibali cha kuanza kazi baada ya kukaguliwa na wahandisi wa mitambo ya radio na elektroniki kutoka TCRA. 
Aidha kipo kituo cha Radio cha Pamoja radio Fm kinachomilikiwa na Mkazi wa Mpanda mjini John Malac ambacho kimekamilika ujenzi kinachosubiriwa ni kibali kutoka tume ya mawasiliano nchini TCRA baada ya marekebisho yalioainishwa na wahandisi kutoka tume. Kituo hiki kipo eneo la Kawajense jirani na ofisi ya Chama cha msingi cha tumbaku LATCU ambapo mwekezaji ameamua kuanza na jingo lililokuwa likitumika kama nyumba ya kuishi na kubadili matumizi yake. 

MWEKEZAJI AWEKEZA KATIKA KISIMA CHA MAJI KAKESE

Baada ya kongamano ndugu Omonyo mkazi wa kijiji cha Kakese Mbugani  aliamua kuwekeza katika sekta ya maji katika kijiji cha Kakese Mbugani kwa lengo la kujipatia kipato kutoka kwa wananchi
Mradi huu umeweza kuondoa kero ya ukosefu wa huduma ya maji safi kwa ajili ya matumizi ya binadamu katika kijiji cha Kakese Mbugani ambapo kilio cha shida ya maji kilikuwa kikubwa kutoka kwa wakazi wa kijiji hicho.
Kwa maelezo yake ni kuwa aliamua kuwa na mradi wa kuuza maji katika  visima viwili virefu vya maji ili kuboresha huduma ya upatikanaji wa maji hapa kijijini pamoja na kujiongezea kipato na ili kutimiza lengo aliamua kuwatumia wataalamu wa maji kutoka halmashauri ya mji. 
Mradi huu umegharamiwa na mmiliki mwenyewe ambapo mpaka sasa mradi huu umetumia shilingi 8,648,500/= hadi kukamilika kwa asilimia mia moja na makusanyo kwa mwezi ni wastani wa shilingi 120,000/= 


KIWANDA CHA KUYEYUSHIA MADINI TPM - MPANDA


Ujenzi wa kiwanda cha kuyeyushia madini mjini Mpanda umeongeza ajira na kipato kwa baadhi ya vijana mjini Mpanda na nje ya Mpanda kutokana na ongezeko la ajira katika kiwanda cha TPM (Tanzania Pema Mining).
Pia mandhari ya mji wa Mpanda imeongezeka ubora na kuwa na uhakika wa soko la madini kwa wachimbaji wadogo  awali walikuwa wakiuza dhahabu kwa bei ndogo kutokana na kukosekana kwa soko la uhakika mjini Mpand.
Katika eneo lilojengewa kiwanda kuna biashara ya mama lishe ambao wamekuwa wakipata kipato kwa njia ya kuuza chakula kwa wafanyakazi wa kampuni ya TPM ambao wanatoka mbali na eneo kiwanda kilipo 
Pamoja na kuwa TPM ilianza kabla ya kongamano la uwekezaji ilikuwepo lakini halmashauri inaamini kuwa uwepo wa kiwanda cha TPM katika mji wa Mpanda ni kivutio kikubwa kwa wawekezaji wengine wa ndani na nje kutokana na kuwepo kwa dhana ya kutokuwezekana mambo katika sehemu kama za kwetu kwa imani tu

KATAVI UNIVERSITY  OF AGRICULTURE (KUA)

 Kuasisiwa kwa mkoa Mpya kumekuja na kuasisiwa kwa ujenzi wa Chuo Kikuu Cha Kilimo ambacho kimepewa jina linalobeba jina la Mkoa na Hifadhi ya Taifa iliyoko katika mkoa yaani Katavi.
Chuo kikuu cha kilimo ni sehemu ya juhudi ya kuwekeza katika Elimu ambapo Halmashauri inaamini kuwepo kwa chuo kikuu kinachomilikiwa na kuendeshwa na Halmashauri kutaiwezesha jamii ya wana Katavi kuwa na maendeleo endelevu na yenye tija katika kuboresha maisha ya wananchi
Chuo Kikuu Cha Kilimo cha Katavi kitaweza kuchangia katika suala zima la elimu ya juu kwa vijana wanaokosa nafasi katika vyuo vikuu vingine kutokana na kuwa ukanda wa Ziwa Tanganyika ni ukanda pekee usio kuwa na chuo kikuu kinachotoa taaluma mbali mbali kwa vijana na wahitimu wa kidato cha sita.    
UWANJA WA NDEGE MPANDA WAWAVUTIA WAWEKEZAJI WA URIC AIR





KAMPUNI YA NDEGE YA URIC AIR YAANZA SAFARI MPANDA‏ 

Wakazi wa mji wa mpanda mkoa mpya wa katavi  wameanza kupata huduma ya usafiri wa ndege tangu mwanzoni mwa mwezi Novemba 2012.
Usafiri huo umeanza kupatikana kufuatia kampuni ya ndege ya URIC AIR kuanza safari ya kusafirisha abiria kutoka Mjini Mpanda kuelekea mikoa mingine.
Ndege hiyo ya kampuni ya URIC AIR itakuwa ikifanya safari zake kila siku katika mikoa ya Mwanza, Katavi na Kigoma ambapo awali wakazi wa mkoa wa Katavi walikuwa wakilazimika kufuata usafiri wa ndege mjini Sumbawanga mkoani Rukwa umbali wa kilometa 240 au mkoani Tabora kilometa 366.
Uwanja wa ndege wa mpanda ambao ni miongoni mwa viwanja vya ndege vilivyotengenezwa kwa kiwango cha lami toka ulipokamilika ulikuwa ukitumiwa na makampuni mbali mbali kutua kwa ndege
Uanzishwaji wa safari za ndege katika mkoa wa Katavi utarahisisha watalii na wawekezaji kufika kwa urahisi mkoani Katavi kwani hapo awali usafiri ulio kuwepo ni wa magari na garimoshi.



KILIMO KWANZA YAJA NA MAPYA MPANDA MJINI

Mradi huu wa matrekta uliibuliwa na vikundi viwili  vya wakulima katika kata za Ilembo na Mpanda Hoteli katika msimu wa mwaka wa fedha 2011/2012 kwa lengo la  kuongeza uzalishaji wa mazao kwa wakulima ambapo matrekta haya yamekuwa yakiongeza ufanisi katika kilimo pamoja na usafirishaji kwa wananchi wenye pato la chini.
Mradi huu unagharana ya shilingi  75,523,160.kati ya hizo Halmashauri ya mji Mpanda imechangia shilingi 1,372,217.00 na vikundi vimechangia jumla ya shilingi 8,200,000.00, mfuko wa maendeleo ya kilimo ASDP umechangia kiasi kilichosalia kwa kwa ajili ya vikundi viwili vya Muungano Farmers Association na Mshikamano Agricultural Group
KATA YA KAWAJENSE YAPATA OFISI MPYA
Katika kuboresha mazingira ya kuhudumia wananchi Halmashauri ya Mji wa Mpanda imefanikisha ujenzi wa ofisi ya Mtendaji wa kata Kawajense na kuondoa kero ya ukosefu wa ofisi kwa watendaji na Diwani wa kata hiyo.
Mradi huu wa ujenzi wa ofisi ya Kata ya Kawajense uliibuliwa na wananchi katika msimu wa mwaka wa fedha 2011/2012 kwa lengo la kuboresha mazingira ya kufanyia kazi na kuongeza ufanisi katika kuwahudumia wananchi kwa gharama ya shilingi 31,001,428 ambapo Serikali kuu imetoa shilingi 21,221,969.50 na wananchi wamechangia jumla ya shilingi 6,019,000
Kata ya Kawajense imekuwa na mahitaji makubwa ya ofisi kutokana na kuwa na eneo la viwanja vipya vya kujenga nyumba vingi kuliko kata nyingine na hivyo kata hii inapokea wageni wengi kila siku hali inayoashiria mahitaji ya ofisi kwa ajili ya kutoa huduma kwa ufanisi.

KARAKANA YA YA WALEMAVU YA KUTENGENEZEA  VIATU  ILEMBO KUKAMILIKA MWAKANI
Halmashauri ya Mji Mpanda inajianda kuendelea na ujenzi wa karakana ya kikundi cha walemavu cha kutengeneza viatu iliyopo katika kata ya Ilembo .
Mradi wa ujenzi wa jengo hili la karakana ulianza mwezi Februari mwaka 2009 kwa lengo la kutoa mafunzo kwa watu wenye ulemavu ili watakapohitimu mafunzo hayo waweze kujiajiri wao wenyewe lakini baada ya kongamano la uwekezaji kikundi cha walemavu waasisi wa karakana hiyo kupitia TASAF waliona umuhimu wa kuanza mikakati ya kukamilisha karakana hiyo ili waweze kuanza uzalishaji kutokana na uwepo wa soko kubwa.
Kupitia halmashauri kikundi hicho kimepata msaada wa kumaliziwa na halmshauri ya mji ili kufikia lengo kabla soko la viatu vya kutengenezwa hapa mjini halijaingiliwa na wazalishaji wengine ambapo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mji, Joseph Mchina alisema kuwa atahakikisha karakana inakamilika kipindi kifupi kijacho kabla ya Oktoba 2013 kwa kutumia fedha za makusanyo ya ndani.
Mradi huu unagharamiwa na wafadhili mbalimbali ambapo mfuko wa maendeleo ya jamii nchini TASAF Umechangia kiasi cha shilingi 9,090,909.90 na  ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Mpanda amechangia shilingi   500,000/=, Mpaka mradi kukamilika utagharimu kiasi cha shilingi 24,000,000/= na halmashauri itachangia gharama zilizobakia ili karakana ikamilika
BARABARA MBILI KUUNGANISHA OFISI YA MKUU WA MKOA KATAVI NA UWANJA WA NDEGE
Katika kuboresha miundombinu ya mji wa Mpanda Halmashauri ya mji iliamua kuweka mazingira mazuri ya miundombinu katika maeneo mbalimbali za mji wa Mpanda ikiwa ni pamoja na barabara ya duara (Ring Road) katika njia ya kwenda ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Katavi kwa kiwango cha lami.
Mradi huu wa ujenzi wa barabara mbili kwa kiwango cha changarawe ulianza mwezi Aprili 25,2012 na unatarajia kukamilika Septemba 25, 2012 kwa lengo la kuboresha miundombinu ya barabara za mjini Mpanda makao makuu ya mkoa wa Katavi.
Mradi huu unagharamiwa na Serikali kuu kwa Tsh. 100,000,000/= ambapo mpaka kukamilika kwa kiwango cha lami zitatumika kiasi cha shilingi 98,463,800/=




WAWEKEZAJI WA KILIMO WAANZA KUJENGA MAGHALA MJINI MPANDA




Katika kuahakikisha uwekezaji katika sekta ya kilimo unakuwa wa manufaa na wa uhakika baadhi ya makampuni yanayowekeza katika kilimo cha tumbaku mkoani Katavi yameanza kujenga maghala ya kuhifadhia mazao yao ili yaweze kuwasaidia katika kuhifadhi mazao.

Kampuni ya kununua tumbaku ya Dmoni ya Morogoro imeamua kuanza kuwekeza katika zao la tumbaku katika mkoa wa Katavi kwa kununua tumbaku kutoka vyama vya msingi kama yalivyofanya makampuni ya TLTC, ATTT na PREMIUM.

Mradi huu una gharama ya shilingi milioni mia tano hadi kukamilika kwa ujenzi wake na  ghala hili linatarajia kuanza kutumika mwakani ambapo lina uwezo wa kuhifadhi tani laki tatu na nusu kwa za mazao kwa wakati mmoja.

CHUO KIKUU HURIA CHACHU YA MAENDELEO YA ELIMU KATAVI









Kuanzishwa kwa Chuo kikuu huria tawi la Mkoa wa Katavi kumetoa fursa ya pekee kwa wananchi wa mkoa huu kuweza kujipatia elimu ya Chuo kikuu kwa gharama nafuu tena katika mazingira yao wenyewe.

Uwekezaji huu wa ni muhimu sana katika kusukuma maendeleo ya wana Katavi kwani Elimu inayotolewa itawasaidia wasio na uwezo wa kifedha na nafasi kupata elimu ya chuo kikuu kwa gharama ndogo na katika mazingira yanayomuwezesha mwananchi wa kawaida kumudu gharama na mahitaji.

Halmashauri ya Mji imekuwa ikiwahamasisha wananchi na wafanyakazi wa taasisi mbali mbali za serikali na zisizo za Kiserikali na kukitumia Chuo Kikuu Huria kujipatia elimu ya Chuo kikuu kwa kutumia mikutano na vikao mbali mbali vya Halmashauri.

UWANJA WA NDEGE MPANDA SASA NI WA LAMI




Maboresho makubwa ya uwanja wa ndege wa Mpanda maarufu kama uwanja wa Kashaulili umefikia hatua ya kiwango cha lami kwa upande wa njia ya ndege na maegesho yake

Kutokana na kuboreshwa kwa uwanja huo sasa ndege zenye uwezo wa kubeba abiria 72 zinaweza kutua katika uwanja huo kwa kipindi chote cha mwaka bila kujali masika au kiangazi

Kukamilika kwa uwanja huu kumeanza kutoa matunda makubwa kwa kuvutia wawekezaji wakubwa na wa kati kuja kuanza shughuli za uwekezaji katika mkoa wa Katavi pamoja na kuibua shughuli mpya za kiuchumi ambazo hapo awali hazikufikirika kama zinawezekana katika mji wa Mpanda na mkoa kwa ujumla.

Baadhi ya shughuli hizo zimewagusa wananchi wa kawaida na nyingine zinawanufaisha pia wawekezaji wengine wa ndani na nje ya mkoa wetu wa Katavi kama vile uanzishwaji wa safari za ndege kwa safari za Kigoma Mpanda Kigoma, Mwanza Kigoma Mpanda na Mpanda Kigoma Mwanza ni sehemu ya faida za kuwepo uwanja bora wa ndege.

HALMASHAURI YA MJI MPANDA YATENGA EKARI 600 ZA KIUCHUMI






Ili kuhakikisha kuwa shughuli za kiuchumi zinapata nafasi katika kipindi cha mapinduzi ya kiuchumi katika mkoa wa Katavi, halmashauri ya mji Mpanda imeandaa ekari mia sita(600) kwa ajili ya eneo maalum la kiuchumi ( Special Economic Zone) katika eneo linalopakana na mtaa wa Airtel.

Eneo hilo litakuwa maalumu kwa ajili ya wawekezaji wa huduma za uwanja wa ndege kama vile maduka vinyago, maduka makubwa (Supermarket), mahoteli na nyumba za kulala wageni zenye hadhi ya kimataifa.

Katika eneo hili kutakuwa na ofisi za makampuni yanayofanya kazi ya kusafirisha watalii katika maeneo yetu ya Kitalii na hifadhi ya taifa ya wanyama ya Katavi.